humph the GREAT
  
 
Waziri Mkuu wa zamani na mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Edward Lowassa
 amesema licha ya changamoto nyingi anazopata akiwa ndani ya upinzani, 
atagombea tena urais katika Uchaguzi Mkuu mwaka 2020 na anaamini 
atashinda.
Lowassa aliyejitokeza kugombea urais kupitia CCM mwaka 2015 na jina lake
 kukatwa kisha kuhamia Chadema alikogombea nafasi hiyo akiwakilisha 
vyama vilivyoungana chini ya Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) na 
kushindwa na Rais John Magufuli, bado anatajwa kuwa mgombea mwenye nguvu
 katika kambi ya upinzani.
Kwa mujibu wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Rais Magufuli alishinda 
kwa kupata kura 8,882,935 sawa na asilimia 58.46, huku Lowassa wa 
Chadema akijipatia kura 6,072,848 sawa na asilimia 39.97 ya kura zote.
Akizungumza jana katika mahojiano maalumu na waandishi wa Nation Media 
Group (NMG) jijini Nairobi, Lowassa alisema, “Kwa mapenzi ya Mungu 
nitajaribu tena mwaka 2020 na nitapita kwa mikono safi.”
Kama ambavyo amekuwa akisema tangu aliposhindwa katika uchaguzi huo wa 
2015, pia jana Lowassa alisema licha ya kuendeshwa katika mfumo 
usioaminika, hakutaka kuwashawishi wafuasi wake wamwage damu kwa kudai 
ushindi.
“Wafuasi wangu walitaka tuingie mitaani kudai ushindi, lakini kulikuwa 
na bunduki nyingi mikononi mwa wanajeshi. Niliogopeshwa na umwagikaji wa
 damu. Sikutaka kuingia Ikulu kupitia damu za watu kwa sababu sistahili 
hivyo,” alisema.
Hata hivyo, alisema licha ya uchaguzi huo kutoaminika, bado anamheshimu 
Dk Magufuli kama Rais, japo mbunge huyo wa zamani wa Monduli alikataa 
kukubaliana na utendaji wa mkuu huyo wa nchi kwa kipindi alichokaa 
madarakani.
“Hata kama Dk Magufuli alichaguliwa katika mfumo usioaminika wa 
uchaguzi, bado tunamheshimu kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa 
Tanzania,” alisema Lowassa. Alisema, “Utendaji wa Rais Magufuli 
utaamuliwa na watu utakapofika mwisho wa muhula huu mwaka 2020. Bora 
niwe makini katika hili nisije nikanukuliwa vibaya nikaingia kwenye 
matatizo nitakaporudi nyumbani.”
Lowassa ambaye hivi karibuni amekuwa akiripoti Makao Makuu ya Jeshi la 
Polisi jijini Dar es Salaam kutokana na kauli yake kuhusu viongozi wa 
Jumuiya ya Uamsho waliokamatwa mwaka 2012 huko Zanzibar, alilaani 
ukiukwaji wa demokrasia akisema Chadema itakwenda mahakamani kudai haki 
ya kufanya siasa.
“Kukataza huko siasa ni kinyume cha demokrasia na haki, hata hivyo 
tunajitahidi kujiimarisha. Tumeshalalamika serikalini kuondoa katazo 
hilo lakini bado inajivuta miguu. Tunaweza kulazimika kwenda kutafuta 
msaada wa Mahakama,” alisema.
Kuhusu kamatakamata ya viongozi wa upinzani, Lowassa alisema licha ya 
kupata zaidi ya kura milioni sita, ameshindwa hata kuwashukuru wananchi 
waliompigia kura.
“Nilipata kura milioni sita na siwezi kufanya mikutano hata ya 
kuwashukuru watu kwa kunipigia kura. Hiyo si tu kinyume cha demokrasia, 
bali si haki,” alisema Lowassa.
Wakati Jeshi la Polisi likikataza vyama vya upinzani kufanya mikutano ya
 hadhara mwaka 2016, Rais Magufuli alisema wanasiasa waliochaguliwa 
wanaweza kufanya mikutano kwenye majimbo yao.
Hata hivyo, bado baadhi ya mikutano ya ndani ya vyama hivyo imeendelea kuzuiwa na viongozi wa upinzani wakikamatwa.
Licha ya kukiri kuwa ndani ya upinzani kuna changamoto nyingi, Lowassa 
alisema kuna wakati anapata faraja kuwa upande huo wa siasa.
“Ni uzoefu mzuri unaoendana na nyakati nzuri na ninafurahia uzoefu huo 
kwa sababu mimi bado ni maarufu na nina wafuasi wengi. Kukataza shughuli
 za siasa ni hatua ya kuninyamazisha,” alisema.
Lowassa alisisitiza msimamo wa Chadema wa kumuunga mkono Rais wa Kenya, 
Uhuru Kenyatta katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Agosti 8 
akisema kiongozi huyo ni chaguo sahihi kwa demokrasia za Kenya.
“Tumekuwa na vikao halali kama chama na vya wazi na kukubaliana kumuunga
 mkono Uhuru Kenyatta achaguliwe tena. Ni mtu mzuri anayeunga mkono 
Jumuiya ya Afrika Mashariki na anaheshimu viongozi wa upinzani,” 
alisema.
Hata hivyo, Lowassa aliyekwenda Kenya kuhudhuria mazishi ya aliyekuwa 
Waziri wa Usalama, Jenerali Joseph Nkaisery alifafanua kuwa uamuzi wa 
kiongozi sahihi wa kuiongoza Kenya utafanywa na Wakenya wenyewe kwenye 
uchaguzi wa Agosti.
Alipoulizwa ni kwa nini Chadema imebadilisha mgombea wanayemuunga mkono 
katika uchaguzi wa Kenya, kutoka kwa Raila Odinga wa Nasa, Lowassa 
alisema amekuwa akimuunga mkono Kenyatta kwa muda mrefu.
Kabla Lowassa hajajiunga na Chadema, Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman 
Mbowe alishatangaza kumuunga mkono Odinga wakati huo akiwa Waziri Mkuu 
wa Kenya.
Akizungumzia kauli ya Lowassa kumuunga mkono Kenyatta, mmoja wa viongozi
 wa muungano wa Nasa, Musalia Mudavadi alimtaka  kiongozi huyo aache 
kuwaingilia katika uchaguzi huo na badala yake apambane na Dk Magufuli 
Tanzania.
Tags
HABARI